Sunday 30 August 2009

“SMZ iwache kushabikia na kuendeleza ubaguzi dhidi ya raia”


TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI 29 Agosti 2009

“SMZ iwache kushabikia na kuendeleza ubaguzi dhidi ya raia”

Kufuatia taarifa iliyochapishwa jana na gazeti la The Guardian juu ya hatua ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ) kuwalazimisha Wazanzibari wenye asili ya Kingazija kwenda kujisajili rasmi kama raia wa Watanzania, Chama cha Wananchi (CUF) kinatoa tamko lifuatalo:

“Kwanza ni kiwango cha juu cha ubaguzi na upotofu kwa SMZ kuendeleza sera zake za kibaguzi dhidi ya Wazanzibari wa makundi tafauti. Misingi hii ya kibaguzi ilianza kujengwa dhidi ya Wazanzibari wenye asili ya Pemba kwa kuwanyima fursa na haki kadhaa za msingi zikiwemo za kielimu, kiuchumi na kisiasa; na sasa baada ya kwisha kuwabagua Wapemba, SMZ inawageukia Wangazija. Serikali ya kweli ya watu haisimamii ubaguzi na utengano, bali mapenzi baina ya watu wake na mshikamano.

“Pili, kisingizio kinachotolea na SMZ kwamba huko ni kufuata sheria iliyotolewa kwa njia ya Dikrii ya Rais tangu mwanzoni mwa Mapinduzi ya Zanzibar na kwamba eti kwa kuwa hiyo ni sheria ambayo haijafutwa kwa hivyo haijatanguka, ni upotofu mwengine wa hali ya juu. Kwanza ilikuwa ni kosa kwa Rais Abeid Karume kutoa tamko hilo ambalo lilikuja kuwa dikrii, kwani aliingiza ugomvi wake binafsi na baadhi ya Wazanzibari waliokuwa na asili ya Kingazija katika masuala ya utawala na khatima ya wananchi. Pili, inasemwa kuwa Mapinduzi yalifanywa kwa lengo la kuwaunganisha Wazanzibari na kufuta misingi ya kibaguzi; kwa hivyo hiyo ilikuwa ni Dikrii iliyokwenda kinyume na misingi ya Mapinduzi na basi ilikosa uhalali tangu mwanzoni.

“Tatu, inaonekana uongozi wa SMZ hauijui hata hiyo jamii ya Wazanzibari unayoitawala. Haijifunzi ukweli kwamba ni mchanganyiko wa asili, makabila, mataifa na historia tafauti ndio ulioifanya Zanzibar kuwa Zanzibar waliyoipata wao (SMZ) kuitawala. Wanapowabagua watu ambao wameleta mchango mkubwa wa kuijenga Zanzibar kijamii, kielimu, kiutamaduni na kisiasa, inafaa Wazanzibari wajiulize tena na tena juu ya aina ya uongozi uliopo madarakani. Ni lazima serikali hii iwache kushabikia na kuendeleza ubaguzi dhidi ya raia.”

Imetolewa na:

Salim Bimani
Mkurugenzi wa Uenezi na Mahusiano na Umma, CUF

Thursday 27 August 2009

Tuesday 25 August 2009

Thursday 20 August 2009

Wapemba watangaza hujuma dhidi ya Masheha na Vingunge wengine...


Huko PBA mambo si shwari kabisa

Kuna madai ya kuibuka kikundi kinachoitwa Hujuma kwa Masheha, ambacho lengo lake ni kudhuru viongozi.

Kundi hilo linalofananishwa na Mungiki la Kenya, limeanza kutoa vitisho kwa kusambaza vipeperushi kwa baadhi ya masheha, kwamba wajiandae kupokea kipigo, huku sheha mwingine akionja adha ya kundi hilo kwa kupambana nalo.

Akizungumza jana, Ofisa Tawala wa Wilaya ya Wete, Khamis Juma Silima, alisema ofisi yake imepokea taarifa za kundi hilo, ambalo lina mrengo wa kisiasa kwa nia ya kuwadhuru masheha hao, kwa madai kuwa ndio kikwazo cha upatikanaji wa fomu za vitambulisho vya Mzanzibari Mkazi, ambazo ni kigezo cha kuandikishwa kwenye Daftari la Kusumu la Wapiga Kura.

Silima alisema masheha kadhaa wamepeleka malalamiko ofisini kwake katika siku za karibuni ya kupokea vipeperushi vya vitisho kuhusu utoaji fomu kwa wananchi wao.

Source: Habari Leo

Tuesday 18 August 2009

Hamad Masauni, na Siasa za kukariri...



Anavyosema kuhusu Pemba ni tofauti sana na hali halisi ya huko Pemba..

Mwenyekiti wa Vijana wa CCM, Hamad Masauni Yusuf alisema ingawa hajui vigezo vilivyotumika katika utafiti, anaamini kuwa wananchi wengi bado wana kasumba kwamba CUF bado ina ngome kubwa kisiwani Pemba wakati hali sasa ni kinyume.

Alisema sio kweli kwamba, CUF wana nafasi kubwa ya kushinda urais kwa Zanzibar na pia huko Pemba na kwamba hali imebadilika kwa sasa akidai kuwa, wananchi wengi wamekata tamaa na viongozi wao na hivyo, CCM ina nafasi kubwa ya kushinda.


Kauli hizi na hali halisi ya huko Pemba ni sawa na kujisuta

Kwa Anayetaka Uprez Zenj...

Saturday 15 August 2009

MMhm Huyu Nae...! CCM Maisara


Mdau wa CCM Maisara, sehemu maarufu hapo Zenj!

Thursday 13 August 2009

Maandalizi ya Kongamano la Kitaifa la Wanablogu



Je wewe ni mwanablogu (Blogger) au mdau wa habari na mawasiliano kwa umma kwa kutumia mtandao? Kama jibu ni ndio, tafadhali unaombwa kujiorodhesha kwa ajili ya maandalizi ya Kongamano Maalumu la Kitaifa kwa ajili Wanablogu (Bloggers) na wadau wa habari na mawasiliano wa Tanzania (Tanzanians Bloggers Summit) linalotarajiwa kufanyika Desemba mwaka huu jijini Dar-es-salaam,Tanzania.

Dhumuni la kongamano hili ni Kuelimishana, Kufahamiana, Kuamsha Utambuzi Rasmi Kuhusu Tekinolojia ya Blogu na Mawasiliano ya Umma kwa Kutumia Mitandao, Kusaidia Utambuzi Rasmi juu ya mchango wa blogu nchini Tanzania kama chombo muhimu cha habari na mawasiliano, Kuelimishana jinsi gani blogu zinaweza kutumika katika kuleta maendeleo katika nyanja za kijamii, kisiasa na kiuchumi, kuburudisha, kukuza utamaduni nk.

Wataalamu mbalimbali kutoka ndani na nje ya nchi wataalikwa kutoa mada na mafunzo mbalimbali kuhusiana na tekinolojia ya kublogu, zana nyinginezo za mawasiliano mtandaoni kama vile mitandao jamii(social networking), online forums nk.Kutakuwa na vipindi vya maswali na majibu.
Ili kufanikisha maandalizi ya Kongamano hili la kihistoria, kujiorodhesha kwako ni muhimu sana. Muda wa kujiodhoresha ni kuanzia tarehe 12/8/2009 (Jumatano) mpaka 12/9/2009 (Jumamosi) tu.

Kinachohitajika ili kujiandikisha ni :
Jina Lako, Anuani yako ya barua pepe (E-mail), Mahali Ulipo au unapoishi (Nchi,mji nk),Namba ya Simu (sio lazima) na Anuani au URL(Universal Resource Locator) ya blogu yako (mfano www.kongamano.blogspot.com/wordpress.com/.com/typepad nk). Vyeti vya Ushiriki vitatolewa kulingana na habari utakazoziorodhesha hapa.
Unaweza kujiorodhesha kwa kutuma ombi lako kwa barua pepe kwenda; summit@bongocelebrity.com.
Zingatia tarehe za kujiandikisha.
Ni mwezi mmoja tu! Asante kwa ushirikiano. UMOJA NI NGUVU!

Bandarini Zanzibar

Wednesday 12 August 2009

Usafirishaji wa Mizigo Zenj...








Usafirishaji wa mizigo kwa kutumia Wanyama ulipigwa marufuku kufanyika ndani ya mipaka ya Halmashauri ya Manispaa ya Zanzibar mara baada ya Mapinduzi. Hata hivyo kidogo kidogo magari ya mizigo ya Punda na Ng'ombe yamerudi tena kubeba mizigo ndani ya Manispaa.




Mkokoteni huko Pemba

Tuesday 11 August 2009

Friday 7 August 2009

Wapemba waendeleza ual-qaeda...!


Baada ya Uchaguzi wa kwanza wa vyama vingi mwaka 1995,Visiwa vya Zenj vilishuhudia vituko kibao, ikiwa ni pamoja na mabomu ya baruti na ya petroli yakilipuriwa katika maeneo mbali mbali ya visiwa hivyo. Toka katika maakazi ya watu, ofisi za serikali na hata sehemu nyeti kama za usambazaji wa umeme visiwani humo zilipata makasheshe ya milipuko ya mabomu. Mabomu mengine yaliweza kulipuka huku mengine yakishindwa kulipuka.

Kipindi hicho kilikuwa ni kabla ya ulipuaji wa mpigo(sambamba)wa mabomu kuanza. Ni katika mwaka 1998 ambao ulipuaji wa sambamba uliponza na kukikuhisha kikundi maarufu cha Al-Qaeda, pale walipoweza kulipua kwa wakati mmoja ofisi ya balozi wa Marekani katika majiji ya Dar es Salaam na Nairobi.

Hapo Majuzi nyumba za Masheha huko Pemba ziliweza kulipuliwa kwa staili hiyo na kufanya wengi kufananisha milipuko hiyo kama ile ya kundi la Al-Qaeda. Huu ni muendeelezo wa ulipuaji wa mabomu huko Pemba kwa madai ya kuwa Masheha wanawanyima wakaazi wa huko kuandikishwa kwenye daftali la kudumu la kupiga kura.

Wapemba katika hili wapo mbele, kwa kumbukumbu za haraka haraka, tokea uchaguzi wa mwaka 1995, kumekuwepo na vituko vingi sana huko Pemba, kama vile vya kugeuza visima vya maji kuwa vyoo, kupaka vinyesi katika skuli,ili kuzuia wanafunzi kusoma, kunyang'nya polisi silaha na kuteka kituo cha polisi, kususia shughuli za maziko na arusi, kubagua watu wa kufanya biashara nao, talaka kwa wanandoa kutokana na tofauti za kisaisa na vituko vingine kaza wa kaza.

Pamoja na yote, ili la mabomu ambalo linaendela sasa, linatakiwa kuchukuliwa hatua za haraka la kulidhibiti, kwani litaweza kuleta madhara makubwa sana hapo mbele, na hasa siku ambayo Wapemba hao watakaweza kuwa na mabomu yenye nguvu(haya ya sasa hayana nguvu kubwa)au mabomu ya sumu! Hivyo basi ni vema kwa vyombo vinavyohusika kuwatafuta watu hawa wanaolipua mabomu na kuwafikisha kwenye vyombo husika. Na ni wakati wa kuanza kuitumia sheria ya magaidi iliyotungwa mara baada ya milipuko ya Dar na Nairobi.

7th August 2009

Nyumba za Masheha wawili zalipuliwakwa mpigo

Milipuko miwili tofauti imetokea sambamba nyumbani kwa masheha wawili kisiwani Pemba na kusababisha zaidi ya watu 30 kunusurika kifo.
Akizungumza na Nipashe juu ya matukio hayo yanayofanana na ile milipuko ya kupanga ya kikundi cha kigaidi cha Al- Qaeda kwa kulipuka kwa wakati mmoja, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kaskazini Pemba, Yahya Bugi, alisema matukio hayo ni ya kupanga.
Alisema katika tukio la kwanza, watu wasiojulikana walitega bomu la kutengenezwa kienyeji kwa kutumia baruti (TNT) na kulilipua nyumbani kwa Sheha wa Mihogoni, Salim Said Salim (59).
Kamanda huyo aliliambia Nipashe kwamba nyumbani kwa Sheha Salim kulikuwa na mkusanyiko wa watu waliokuwa wakihudhuria harusi nyumbani kwake saa sita usiku wa kuamkia jana.
Alisema bomu hilo lililipuka wakati Sheha na wageni wake wakiwa wamelala na kusababisha athari kubwa kwenye ukuta wa nyumba yake na mabati sita yaliyoezekwa nyumba hiyo kung’oka.
Kamanda Bugi alisema kwa mujibu wa Sheha Salim, walisikia kishindo kikubwa kikitokea nyuma ya nyumba yao na baada ya kukimbilia katika eneo hilo waliwaona vijana wawili wakikimbilia eneo lenye migomba.



Zaidi: tembelea Nipashe

Thursday 6 August 2009

Pinda amefulia...


Kwa kauli yake juu ya Muungano Waziri Mkuu Mizengo Pinda amefulia na ameonyesha ufahamu mdogo juu ya Muungano huu. Kauli yake ya kuondoa kero za muungano ni kuifuta SMZ haiwezi ikaachwa hivi hivi. Kauli ambayo aliitoa huku akijua kuwa hakuna dalili zozote za sasa za SMT kujaribu kuondoa kero za Muungano achilia mbali jitihada za kuona kuwa Muungano unakwenda vizuri zaidi ya kuburaza upande mmoja wa Muungano. Kauli yake inaweza kuwa sahihi iwapo Muungano huu utakuwa hauna kero yoyote na nchi zote mbili kuridhia kuwa hakuna kero.

Zaidi Pinda anahitaji kupatiwa tuition ya haraka kuhusu Muungano na mambo yote ambayo yahusianayo na Muungano huo. Hii itamuwezesha kujua na kupata ufahamu mkubwa wa Muungano huu kabla ya kujikuta akishitumiwa na kuandamwa na Katiba na kukimbilia kulia.

Wednesday 5 August 2009

Tuesday 4 August 2009

Mwakilishi adai wizi wa watoto umekithiri Zanzibar


WAJUMBE wa Baraza wameishauri Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kufuatilia kwa kina upoteaji wa watoto katika maeneo mbalimbali pamoja na kushughulikia suala la utumiaji wa dawa za kulevya nchini.

Walitoa ushauri huo jana walipokuwa wakichangia makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara ya Kazi Maendeleo ya Vijana, Wanawake na watoto kwa mwaka wa fedha 2009/10 katika kikao cha baraza la wawakilishi kinachoendelea Mjini Unguja.

Mwakilishi kupitia Wanawake (CCM), Raya Suleiman Hamad, alisema kuna haja kwa serikali kuanzisha uchunguzi huo kwani watoto wengi wanapotea ovyo katika mitaa yao, huku wazazi wao wakiwa wanahangaika kuwatafuta bila ya mafanikio.

Alisema kwamba inavyonekana wapo baadhi ya watu wanaoendesha biashara ya kuiba watoto jambo ambalo tayari limeanza kuwatia hofu baadhi ya wazazi nchini.

Mwakilishi huyo alisema kwamba watu wanaoendesha vitendo hivyo hutumia njia za kuwahadaa kwa kuwafuata watoto na kuwapa fedha kisha wanawasihi wawafuate ili wakawanunulie nguo.

Mwakilishi huyo alitoa mfano katika mtaa wa Nyerere kwamba kuna kesi za kupotea watoto wanne na kwamba hadi sasa hawajapatikana pia hawajulikani walipotea katika mazingira gani.

Aliitaka serikali ichukue hatua za kufanya utafiti juu ya suala hilo kwa vile tayari limeanza kuwatisha wananchi na linaweza kusababisha madhara makubwa baadaye

Alisema wakati serikali ikilitafakari hilo, ni vyema hivi sasa kuangaliwa uwezekano katika bandari na Viwanja vya Ndege watu wanaoonekana kubeba watoto wakahojiwa uhalali wao.

Mwakilishi huo pia alizungumzia suala ubakaji wa watoto kuendelea ikiwa pamoja na wagonjwa wa akili na kutaka vyombo vya sheria kutekeleza majukumu yao bila ya upendeleo kwani matendo kama hayo yakiachwa yanaweza kuhatarisha usalama kwa watoto .

Akitoa mifano Mwakilishi huyo alisema iliyowahi kujitokeza kisiwani Pemba baada ya mtoto mmoja kubakwa lakini kesi yake ilipopelekwa Polisi wamekuwa wakishindana na Polisi kwa kuwaeleza wahusika hawana la kufanya na waende wakamkamate mhusika wampeleke kituoni hapo.

Mwakilishi huyo pia alisema ni lazima serikali iandae mkakati maalum wa kukabiliana na tatizo hilo kwani suala la madawa ya kulevya linaonekana kama vile limeshindikana kutokana waletaji na wauzaji wa dawa hizo kuwa wanafahamika lakini hawachukuliwi hatua zozote za kisheria wakati vijana wengi wanazidi kuharibika na utumiaji wa madawa hayo.